Raia watatu wa Uganda wameishtaki mamlaka ya dawa nchini humo pamoja na shirika la kimataifa la Marie Stoppes kwa kupata magonjwa ya zinaa na ujauzito baada ya kutumia kondomu ambazo hazikuwa na ubora.
Taasisi hiyo isiyokuwa ya kiserikali ilisambaza kondom ambazo baadae mamlaka ya dawa ilisitisha matumizi yake mwaka 2019.
Mwanaume mmoja alidai kuwa alitumia kondomu ya 'Life Guard' lakini wakati wa kujamiiana ilipasuka na hivyo kumsababishia kupata virusi vya Ukimwi huku mwingine alidai kuwa alipata ugonjwa wa zinaa wa gonorea.
Na mwanamke mmoja alisema kuwa alipata ujauzito baada ya kutumia kondomu hiyo.
Madai dhidi ya kondomu hizo yalidai kuwa hazikupimwa na kuthibitishwa ubora wake kabla ya kusambazwa kwa umma.
Marie Stoppes ilisambaza kondomu milioni mbili kwa mwezi katika nchi nzima.
Inaonekana kuwa uingizwaji na usambazaji wa kondomu hizo ulisitishwa.
Mamlaka ya dawa ya taifa na wahusika wote wa kuthibitisha ubora wa bidhaa za afya wanalalamikiwa kwa kushindwa kutimiza majukumu yao kabla ya kusambazwa kwa kondomu hizo sokoni
Awamu mbili za ugawaji wa kondomu zipatazo milioni moja, zilisitishwa sokoni na serikali mwezi Novemba 2019, kufuatia malalamiko kutoka kwa Umma.
Lakini wengi wameuziwa kondomu hizo na asilimia 70 tu ndio ziliweza kuondolewa sokoni.
Aidha, wanaume wawili waliishtaki Marie Stoppes kwa madai mengine mwezi Februari mwaka huu, wakitaka fidia.
Chanzo: BBC Swahili
Tags
BREAKING NEWS