TAKUKURU WAONESHA RUSHWA YA NGONO ILIVYOKITHIRI VYUONI

MBINU inayoongoza kutumiwa na baadhi ya wahadhiri, kushawishi wanafunzi wa vyuo vikuu watoe rushwa ya ngono ni tishio la kuwapa alama za chini kwenye mitihani, imefahamika.


Mbinu nyingine wanayotumia wahadhiri hao ni kujiunga kundi moja la whatsapp na wanafunzi na wahadhiri; na vitisho wanavyotoa kwa wanafunzi hao vya kutofaulu kabisa masomo husika.


Hayo yamebainishwa kwenye ripoti ya utafiti uliofanywa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuhusu tatizo la rushwa ya ngono katika vyuo vikuu viwili vya umma nchi, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu Cha Dodoma (UDOM).


Utafiti ulifanyika kwenye vyuo hivyo kutokana na ukongwe UDSM, lakini pia idadi kubwa ya wanafunzi wanaodahiliwa na vyuo vyote viwili kwa mwaka.


Kwa mujibu wa ripoti hiyo, watumishi 65 sawa na asilimia 29.9 na wanafunzi 174 sawa na asilimia 18.7, walieleza kuwepo kwa ushawishi wa makusudi ili kujipatia huduma kutoka kwa wenye mamlaka.


Takwimu za utafiti huo zinabainisha kuwa mbinu ya vitisho vya alama za chini kwa UDSM iliongoza kwa asilimia 40.5 na UDOM asilimia 38.6, vitisho vya kufeli mitihani ilifuatia kwa asilimia 28 UDSM na asilimia 31.1 UDOM.


Kwa mujibu wa utafiti huo, mbinu nyingine zinazotumika ni pamoja na ahadi ikiwemo ya kuolewa, cheo, chumba chuoni, nafasi ya uongozi, na kuongezewa alama za ufaulu.

Aidha, imebainika kuwa ushawishi wa makusudi kufanya ngono kufanyika kwa asilimia 26.5 UDSM na asilimia 22.4 UDOM.


Aidha, utafiti huo ulibainisha mbinu nyingine zinazowaingiza mtegoni wanafunzi kwenye vyuo hivyo kuwa ni wahadhiri kuwaita wanafunzi kwenye mazingira yasiyo rasmi kwa ajili ya kukagua utafiti inayofanyika kwa asilimia 3.9 UDSM na asilimia 7.5 UDOM.


Mbinu nyingine wanayotumia wahadhiri ni kujiunga kundi moja la whatsapp na wanafunzi, na imefahamika kuwa hilo kufanyika kwa asilimia 1.1 UDSM na asilimia 0.6 UDOM.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, utafiti unaeleza kuwa wahadhiri wanafahamu kwamba mwanafunzi anakuja chuoni kwa lengo kuu la kupata tuzo za kitaalum,a hivyo hutumia mwanya huo kwa kuwapa alama ndogo za masomo, kubadilisha alama za ufaulu, kuwafelisha au kuzuia matokeo yao ili kuandaa mazingira ya kuwashawishi kingono.


“Kuwepo kwa ucheleweshwaji wa fomu za mikopo kwa makusudi au jina la mwanafunzi kurukwa ili malipo yake yasikamilike kwa wakati. Hii imekuwa moja ya njia wanayoitumia kushawishi rushwa ya ngono” hiyo ni sehemu moja ya shuhuda kwenye ripoti hiyo.


Ushuhuda mwingine ulionukuliwa kwenye ripoti iyo ya utafiti ni “Mwanafunzi alitakwa kingono na mhadhiri akamkatalia, baada ya kumkatalia mwanafunzi alianza kuona madhara yake kwa kuwekewa alama za chini”


Nukuu nyingine ya ushuhuda wa vitisho vya kushawishi rushwa ya ngono ni “Mhadhiri aliomba rushwa ya ngono kwa mwanafunzi aliyekuwa amefaulu mtihani wa majaribio (test) alikuwa amepata alama 84…lakini mhadhiri hakumrudishia karatasi yake ya mtihani na kumweleza kuwa amefeli mtihani na hivyo yuko tayari kumwongezea alama hadi zifike 84 iwapo atampa rushwa ya ngono,”


Kwa mujibu wa utafiti huo, mwanafunzi huyo alipoenda ofisini kwa mhadhiri, alimkuta yuko na mhadhiri mwingine na alipoomba karatasi yake alikataliwa, kwa madai kwamba yupo kwenye mazungumzo.


“Kwa bahati mhadhiri mwenzake bila kujua kinachoendelea alimshauri mhadhiri huyo amsikilize mwanafunzi, ndipo alipatiwa karatasi yake na kubaini kuwa alikuwa amefaulu kwa kupata alama 84,” ilibainisha ripoti hiyo.


Ushuhuda mwingine uliobainishwa kwenye ripoti hiyo ni kuwepo tabia ya baadhi ya wahadhiri kuwatongoza wanafunzi mapema wanapofika kuanza masomo chuoni kwa njia mbalimbali, zikiwemo kuwapigia simu na kuwatumia ujumbe mfupi wa maneno kupitia simu za kiganjani.


“Wanafunzi wanapokataa wahadhiri hao huwatishia kuwa watahakikisha hawafaulu katika masomo wanayofundisha...kuna wanafunzi walilalamika kwa uongozi wa chuo kutokana na kukataa kutoa rushwa ya ngono kwa mtuhumiwa uongozi wa chuo ulielekeza usahihishaji wa somo hilo ufanyike upya na matokeo yalionesha kuwa wanafunzi hao walifaulu, uongozi ulichukua hatua za kiutawala dhidi ya mtuhumiwa,” ilisema sehemu ya ushuhuda katika ripoti hiyo.


Ripoti hiyo inaeleza kuwa matokeo hayo, yanaonesha kuwepo kwa vitendo vya makusudi vya baadhi ya wahadhiri kulazimisha ngono kwa wanafunzi.


“Vitendo hivyo vinakiuka kifungu cha 25 cha sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa namba 11 ya mwaka 2007. Sheria hii inaharamisha kitendo chochote cha mtu mwenye mamlaka kumuwekea kigezo cha ngono mtu yeyote anayetaka huduma yake,” ilieleza ripoti hiyo ya Takukuru.



#HabariLeo





Post a Comment

Please Select Embedded Mode To Show The Comment System.*

Previous Post Next Post

Disqus Shortname

sigma2

Contact Form